Tuesday 18 August 2015

SI RAHISI

Si rahisi, si rahisi, si rahiiisi!
Kuamua niwaambieni, kumtumikia Mterehemezi,
Kwa moyo wako kumfuata, akili yako kumuwaza,
Ni jambo muhali niwaambieni, tunaloliona hivi sasa.
Vijana barobaro, kutoasi ukapera,
Kuwaacha wao mademu, wamsake wao Mungu,
 Wasifurahie hiyo ndoa, isiyo hata doa,
Ni jambo muhali niwaambieni, tunaloliona hivi sasa.

Wasichana pia nanyi, kutawazwa mchongoma,
Yahitaji kwingi kujitolea, kuamua liwe liwalo,
Utajitoa mhanga kweli, uumche wako Muumba,
Umtumikie kwa miaka, mikaka si haba,
Ni jambo muhali niwaambieni, tunaloliona hivi sasa.



Wazazi kuitikia, chao kitoto kiwaage,
Walikipakata wakaklilea, kunyonya kikanyonya,
 Kusoma kimesoma, kunenepa kikanona,
Wangetaka kweli sana, kiwalipe yao fidia,
Kiwazae wajione, waitwe “Daddie” na pia “Mummie”,
 Ni jambo muhali niwaambieni, tunaloliona hivi sasa.


Hata hivyo tusiasi, atuitapo tuitike,
Tusije kataa wito, tukatae atuitialo,
Sisi mabarobaro, dunia kombokombo,
Yahitaji yetu nishati, masikini wapate shati,
Twaweza na tutaweza, kipawa tumepewa,
Ijapo jambo muhali, kwa Mungu hamna ghali.


Tamati nifikapo, mkazo natilia,
Mungu natumuombe, tujue wetu mustakabali,
Atufunulie yetu njia, tuifuate aitakayo,
Akitaka uwe padre, usikatae kaka,
Akiamua uwe mtawa, tawika dada,
Ijapo jambo muhali, kwa Mungu hamna ghali.



James Njenga

No comments:

Post a Comment